Maelezo ya onyo, "cautioned statement" ni maelezo ambayo hutolewa kituo cha polisi na mtuhumiwa wa kosa la jinai baada ya kuwa amefahamishwa na afisa wa polisi anayemhoji kwamba, "halazimiki kujibu swali lolote atakaloulizwa na afisa polisi, tofauti na swali linalotafuta habari kuhusiana na jina na anuani yake", na "anaweza kukataa kujibu swali lolote atakaloulizwa na afisa polisi". Na kwamba maelezo yake yanaweza kutumiwa kama sehemu ya ushahidi mahakamani.
Baada ya hatua hiyo, mtuhumiwa anaweza kutoa maelezo yake kwa njia ya mdomo kisha kuandikwa na afisa wa polisi, au anaweza kuandika maelezo hayo kwa mkono wake na kukabidhi kwa afisa wa polisi.
Baada ya maelezo kuchukuliwa kwa maandishi, afisa wa polisi atalazimika kuyasoma maelezo hayo kwa mtuhumiwa au kufanya maelezo hayo yasomwe kwa mtuhumiwa, au kumpa mtuhumiwa asome maelezo aliyoyatoa, Kisha mtuhumiwa anaweza kurekebisha makosa katika maelezo yake.
Mtuhumiwa atasaini maelezo yake kuthibitisha kuwa ameyasoma maelezo hayo, mtuhumiwa hatakiwi kutoa maelezo kwa kulazimishwa kwa kupigwa au njia yoyote nyingine tofauti na njia za kisheria.
Pale mtu anapokuwa kizuizini, afisa polisi hatamuuliza maswali yoyote, au kumtaka kufanya chochote, kwa madhumuni yanayohusiana na upelelezi wa kosa, isipokuwa kama:–
(a) afisa polisi amemwambia jina na cheo chake;
(b) mtu huyo amejulishwa na afisa polisi, katika lugha ambayo anaielewa, kwa maandishi na, kama inawezekana, kwa mdomo, kwamba yuko kizuizini na kosa ambalo kwalo yupo kizuizini; na mtu huyo ameonywa na afisa polisi katika hali ifuatayo, yaani, kwa kumjulisha au kusababisha kujulishwa, katika lugha anayoielewa, kwa maandishi kwa kufuata fomu iliyowekwa na, iwapo inawezekana, kwa mdomo kwamba;
(i) halazimiki kujibu swali lolote atakaloulizwa na afisa polisi, tofauti na swali linalotafuta habari kuhusiana na jina na anuani yake; na
(ii) kwa kuzingatia Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, anaweza kuwasiliana na mwanasheria, ndugu au rafiki.

0 Maoni
WEKA MAONI YAKO HAPA.
TAFADHALI USITUMIE LUGHA YA MATUSI AU KUUDHI KWANI NI KOSA KISHERIA.
KARIBU SANA NA ASANTEE.. 🇹🇿